MTIHANI MPYA KIDATO CHA NNE HUU HAPA, KUSAMBAZWA MEI 10

Wanafunzi wa Kidato cha Nne, watafanya mitihani miwili ya Taifa mwaka huu, baada ya kuongezwa mtihani wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN), ambao utatumika kuwapima walivyojiandaa na Mtihani wa Taifa wa Kumaliza Elimu ya Sekondari.
Mkurugenzi wa Elimu ya Sekondari, Paulina Mkonongo, alitangaza utaratibu huo jana na kufafanua kwamba lengo ni   kubaini wanaohitaji msaada kabla ya mtihani wa mwisho, ili kuboresha taaluma darasani. 
Kwa mujibu wa Paulina, mtihani huo wa BRN, utafanyika kwa masomo machache lakini yanayosomwa na wanafunzi wote ambayo ni Baiolojia, Hisabati, Kiswahili na Kiingereza.
Paulina alisema mtihani huo wa majaribio, tayari umeanza kuandaliwa na utasambazwa kwa maofisa Elimu nchini ifikapo Mei 10 mwaka huu, na barua kuhusu kufanyika kwa mtihani huo imeshatumwa kwa makatibu tawala wote, ili kuanza maandalizi.
Matokeo ya mtihani huo, yanatarajiwa kutumika kubaini mada ngumu kwa wanafunzi,  wanaohitaji msaada na kuwapa walimu mwanga kuhusu wapi wanafunzi hao wanahitaji msaada na lengo ni kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.
Tayari  tangu mwaka jana mikoa 12 ilianza kushiriki katika programu iliyohusisha mafunzo kwa walimu 4,064 wa masomo husika, na mikoa 13 iliyosalia itashiriki programu hiyo mwaka huu. 
Mafunzo ya walimu wa mikoa hiyo 13 kwa mujibu wa Paulina, yatafanyika Juni 2014 na programu ya mafunzo rekebishi kwa wanafunzi wenye upungufu, itaanza Julai mwaka huu kulingana na matokeo ya mtihani watakaofanya.
“Tutatoa mtihani wa majaribio kwa wanafunzi wa kidato cha nne, ili kubaini maeneo yenye wanafunzi wanaohitaji msaada zaidi na kutoa utaratibu wa mafunzo rekebishi na mafunzo kazini,  ili kuwajengea uwezo walimu wa kuwasaidia wanafunzi walioko kwenye hatari ya kutofanya vema,” alisema Paulina.
Hata hivyo, Paulina alisema katika utekelezaji utoaji wa mtihani huo, wanakabiliwa na changamoto ya kuwapatia mafunzo wakuu wa shule zisizo za serikali, kuchapisha kitabu cha mwongozo na ziara za wasimamizi wa elimu katika ngazi mbalimbali kutoa ushauri.
Tayari walimu wakuu 3,001 wa shule za Serikali wamepatiwa mafunzo na Taasisi ya Uongozi wa Elimu Bagamoyo (ADEM) katika maeneo yaliyoainishwa, huku kitabu hicho cha mwongozo kikiwekwa kwenye tovuti ya Wizara.
Paulina alisema mikakati endelevu iliyopo, inalenga kuendeleza mafunzo ya walimu kazini, ili kuwajengea uwezo kulingana na wakati na mahitaji ya mitaala.
Mbali na mafunzo hayo, pia wanalenga kuwajengea walimu tabia ya kutunga mitihani bora ya kupima mchakato wa ufundishaji, kubaini wanafunzi wanaohitaji kusaidiwa zaidi, kubaini mada ngumu na kutoa mafunzo rekebishi kwa wanafunzi.
Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Dk Charles Msonde, alisema vitabu rekebishi vitaonesha wanafunzi waliofanya vizuri katika kila swali, waliojibu vibaya na swali lilikuwa likitaka nini.
Vitabu hivyo vitasaidia walimu na wanafunzi kubaini makosa mbalimbali yanayofanywa na watahiniwa wakati wa kujibu maswali na kutumia mbinu bora za kujibu maswali.
“Mwisho wa vitabu hivyo, kuna mada zilizofanywa vizuri na vibaya na jinsi ya kusaidia walimu wahakikishe wanafunzi wanafaulu mada hizo,” alisema.
Vitabu hivyo kwa shule za msingi vimetolewa vya masomo ya Kiswahili, Hisabati, Kiingereza, Sayansi na Maarifa ya Jamii kwa ajili ya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2012 na 2013.
Kwa sekondari, vimetolewa kwa masomo ya Hisabati, Uraia, Historia, Jiografia, Kiswahili, Kiingereza, Baiolojia, Kemia na Fizikia kwa mwaka huo.
Dk Msonde alisema Baraza pia limepewa jukumu la kupanga shule katika makundi ya ubora wa ufaulu, ili kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule za msingi na sekondari, na kuwajengea walimu na wanafunzi hali ya ushindani na kujitambua kama shule imepanda au imeshuka.
Makundi ya ufaulu yatapangwa kwa kutumia rangi za kijani kwa shule zenye ufaulu wa juu, njano kwa zenye ufaulu wa kati na nyekundu kwa shule zenye ufaulu wa chini kwa shule za msingi na sekondari.

No comments: