MAHAKAMA YAWAACHIA HURU VIGOGO SABA WA SUMA JKT

Vigogo saba wa Shirika la Uchumi la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT) waliokuwa wanakabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya madaraka, wameachiwa huru katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Hakimu Mkazi Aloyce Katemana alitoa uamuzi huo jana kwa kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imeshindwa kuthibitisha mashitaka dhidi ya washitakiwa hao.
Washitakiwa walioachiwa huru ni Mkurugenzi wa Shirika hilo, Kanali Ayoub Mwakang’ata, Luteni Kanali Mkohi Kichogo, Luteni Kanali Paul Mayavi, Meja Peter Lushika, Kanali Felix Samillan, Sajenti John Laizer na Meja Yohana Nyuchi.
Walikuwa wanakabiliwa na mashitaka saba ya kula njama, kutumia vibaya madaraka yao  kwa kutoa uamuzi wa ununuzi wa vifaa chakavu vya ujenzi bila kibali kutoka bodi ya wakurugenzi wa Kampuni ya  TAKOPA  ambao imeundwa kwa ubia wa Suma JKT na kampuni nyingine ya Korea. Pia walidaiwa kuhamisha  fedha kinyume cha sheria.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Katemana alisema Takukuru wameshindwa kueleza jinsi washitakiwa hao walinufaika  kutokana na kutoa uamuzi huo wa kununua vifaa hivyo chakavu.
Alisema  kwa mujibu wa ushahidi washitakiwa hao walifuata taratibu zote, walikaa kwenye vikao husika na kutekeleza matakwa ya wanahisa ambao ni Suma JKT pamoja na kampuni ya Korea.
Katika mashitaka ya kuhamisha Sh bilioni 3.8 kutoka katika akaunti ya Takopa kwenda Suma JKT, yaliyokuwa yanawakabili Kanali Samillan na Luteni Kanali Kichogo, Hakimu Katemana alisema Takukuru wameshindwa kueleza washitakiwa hao walipata manufaa gani baada ya kuhamisha fedha hizo.
Alisema washitakiwa hao hawakutumia vibaya madaraka yao bali walifuata taratibu kwa sababu walikuwa wanatekeleza majukumu yao kama watia saini wa Takopa na hakuna ushahidi ulioonesha walipata manufaa yoyote kutokana na kitendo hicho.
Aliongeza kuwa ili mtu awe ametumia madaraka vibaya ni lazima afanye jambo kwa lengo la kujipatia faida lakini ushahidi uliotolewa mahakamani hapo haujaonesha kama washitakiwa walinufaika hivyo mahakama inawaona hawana hatia.
Katika kesi hiyo, Takukuru walikuwa na mashahidi 10 pamoja na vielelezo 25, upande wa utetezi walikuwa na mashahidi tisa na vielelezo vitano.
Washitakiwa wakiwa wajumbe wa Bodi ya Tenda ya SUMA JKT, walidaiwa kutumia vibaya madaraka kwa kutoa uamuzi wakidai ulitolewa na TAKOPA kwa ajili ya kununua magari na vifaa chakavu vya ujenzi bila kupata idhini ya kutoka Bodi ya Wakurugenzi wa TAKOPA.
Inadaiwa vifaa hivyo vilinunuliwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Msata hadi Bagamoyo, baada ya kampuni ya Takopa ambayo ni ya ubia kati ya Suma JKT inayomiliki hisa 30 na kampuni ya Korea yenye hisa 70, kupata zabuni ya ujenzi huo.

No comments: