WANAFUNZI WA KIKE SEKONDARI YA MZINDAKAYA WADAIWA KUWEKWA KINYUMBA...

Baadhi ya wanafunzi wa kike wakifua nguo zao.
Baadhi ya wasichana  wanaosoma katika Shule ya Sekondari Mzindakaya iliyopo kijiji cha Kaengesa, wilayani Sumbawanga, wametajwa kuishi kinyumba na wanaume ambao huwahudumia kwa kuwapatia  mahitaji muhimu  ikiwemo  chakula, mavazi  pia vileo.

Wanafunzi hao ni wale wanaoishi nje ya hosteli za shuleni hapo, wakidai wazazi wao hawana uwezo wa kulipa gharama za hosteli na hivyo kuamua kupanga vyumba maarufu kama 'magheto' nje ya maeneo ya shule.
Uchunguzi  uliofanywa na mwandishi hivi   karibuni  kijijini  hapo ilipo shule hiyo,   ikiwa  ni umbali  wa  zaidi ya  kilomita  40 kutoka  mjini Sumbawanga  umebaini  kuwa  baadhi ya  wanafunzi  hao  wa  kike kutokana na kuwa huru kupita kiasi  kwa  kuishi katika 'magheto'  wamejingiza  katika 'ufuska' na ulevi  wa pombe   wa  kupita  kiasi.
"Si  ajabu  kukutana  kijijini hapa  siku  za  wikiendi  na msichana  wa shule  akiwa  amelewa  pombe. Watoto  hawa  kwa  kweli  wameshaharibikiwa wengine  ni walevi  kupindukia," alisema  mama mmoja  kijijini hapo  ambaye hakuwa  tayari  jina lake kuandikwa   gazetini.
Pia  uchunguzi  wa  mwandishi  umebaini kuwa kuna mwingiliano  mkubwa  wa  vijana  wa kiume  kijijini hapo  wakitokea  ndani na nje ya mkoa ambapo  baadhi yao wanafanya vibarua   katika  kampuni  ya ujenzi  wa  barabara  ya Laela  hadi  Sumbawanga  mjini  ikipitia kijijini  hapo  yenye umbali wa  kilomita  97 kwa kiwango  cha lami.
Wengine  wanadai  kuwa  ni  walanguzi  wa mazao  ya nafaka  hususani  mahindi,  lakini  pia wapo  vijana ambao  ni maarufu kama  wezi  wa  mafuta  wanaodaiwa  kuiba  nishati hiyo  ya kuendeshea  mitambo  na magari  kutoka  katika  Kampuni hiyo  ya ujenzi  wa barabara hiyo  kisha  kuyauza  kwa  madereva  wa magari makubwa  na madogo  kwa bei   rahisi.
Inadaiwa kuwa  kutokana  na vijana hao  wa kiume  kuwa na uwezo  fulani wa kifedha, huwapatia fedha  vijana wa kiume  wakazi wa kijijini hapo ili wawaunganishe na wasichana hao  wanafunzi wanaoishi katika magheto.
Kwa mujibu wa  baadhi  ya  vijana wa kiume  walihojiwa na  mwandishi  wa habari  hizi  wamekiri kuwa  kuwarubuni wasichana  hao kuwahonga  chakula, nguo  pia kuwashawishi  kunywa   pombe  ambapo  baadhi yao  wamejikuta  wakiishi  nao  kinyumba  kwa  kuwapangishia  nyumba  kijijini  hapa  huku wakiendelea  na masomo yao shuleni  hapo  kama kawaida .
"Hawa  wanafunzi wa kike  wanaishi  katika  'magheto' wako  huru  sana   hivyo  kujikuta  wakijiingiza  katika  tabia  mbovu,  zikiwemo  za ukahaba,  fikiri  mwanafunzi  wa kike  kunywa  pombe  isitoshe hapa  kijijini  kuna  nyumba  za kulala  wageni  hakuna anayewazuia kulala  humo na wanaume," alisema  kijana moja wa kiume   kwa masharti ya  kutoandikwa  jina lake.
Watoa  taarifa  hao  kwa masharti ya kutoandikwa  majina  yao wamekiri kuwa  wanaume  wanaishi  na  wasichana hao  kinyumba  kwa siri,  kwani  huingia  kwenye  vyumba  vya  wasichana  hao  usiku  kwa siri  na alfajiri  huondoka  na kurejea  wanakoishi ambapo  wasichana nao  hujiandaa  kwenda shuleni.
Lakini  pia uchunguzi  wa mwandishi umebaini kuwa  si wanafunzi  wote  wanaishi  kwa kupanga vyumba  kijijini humo   wanatoka  katika familia  masikini,  lakini  pia  wapo  ambapo  wazazi  wao  wanaojimudu  kiuchumi  na  kuwachangia  gharama za kuishi  hosteli,  lakini  hukacha  na  kuishi  kwa kupanga  nyumba  kijijini   ili  waweze kuwa  huru  zaidi .
Akizungumza  na  mwandishi  wa habari   hizi  hivi  karibuni  shuleni hapo, Makamu  Mkuu  wa shule hiyo, Agatha Okumu  amekiri kuwa  si  salama kabisa  kwa  wasichana  hao  kuishi  kwa  kupanga  vyumba  kijijini  hapo  wakati  mabweni yapo  shuleni hapo  kwa ajili  yao.
"Kutokana  na kuishi  kwa  kupanga  vyumba  kijijini  hapa  wanafunzi  hao wa kike  wamejikuta  wakivamiwa  na  watu  wasiojulikana  usiku  wakiwa  wamelala  na  kuwafanyia  vitendo  vya  udhalilishaji  ikiwemo  kubakwa lakini hawasemi wanakaa kimya kisa eti wanaona aibu kusema kuwa wamebakwa.
Pia alikiri kuwa   baadhi ya  wazazi na walezi  wanagoma  kuchangia  gharama  za watoto wao kuishi  hosteli  shuleni hapo   hivyo wanafunzi  hao  wanalazimika   kupanga vyumba  kijijini humo ambapo  kodi  ya chumba kwa mwezi ni  Sh 1,000-  hivyo  kujikuta  wakijiingiza  katika  tabia  mbaya na  baadhi yao  wakishia kudhalilishwa  kijinsia .
Naye Mkuu wa Shule  hiyo, Nicholas  Thomas  alisikitishwa  na  wazazi   wa watoto  hao  wa kike  kukataa  kuchangia gharama ili  watoto  hao  waweze kuishi  katika hosteli  shuleni  hapo,  kwa  madai  kuwa  wao  ni  masikini  hawana  uwezo  wa  kuchangia magunia  mawili  ya mahindi, debe moja la maharage na Sh 40,000  kwa  mtoto  mmoja aishi  bweni  kwa muhula mmoja .
Kwa mujibu  wa  Mkuu huyo wa Shule, yapo  mabweni  mawili   ambao  yana  uwezo  wa kuchukua  wanafunzi  wa kike zaidi ya 200, lakini  vyumba vingi  viko  wazi  kwa kuwa   wengi wao  wamepanga  vyumba  kijijini.
"Shule  hii  ina wasichana  240  acha  wavulana  lakini  wanaoishi  hosteli  ni 83  tena  wameongezeka  hivi karibuni  baada  ya  wazazi  wao  kuvuna mazao   shambani.  Wazazi   ni wagumu  wanadai  wao  ni maskini  hawawezi  kumudu   kuchangia gharama  za  watoto  wao  kuishi  hosteli  shuleni hapo tatizo  hakuna sheria  inayowabana," alisema.
Baadhi  ya wanafunzi  wa kike  wa shule  hiyo  waliohojiwa na  mwandishi wa habari   hizi  wamekiri  kuwepo  kwa  tabia hiyo  waliyoiita 'chafu'  miongoni  mwao,  lakini  pia  wanawalaumu  wazazi  wao  kwa kushindwa kutimiza wajibu  wao  kama wazazi  wao  kwamba 'wamewatelekeza'  kwa kukataa  kuwagharimia ili waweze kuishi  bwenini  shuleni hapo  kwenye usalama  na malezi  mazuri .
"Wazazi  wetu si  maskini  kiasi  hicho  wametutelekeza sana  na  kutuacha  kwenye" midomo  ya simba  tunakoishi  kwenye  magheto si salama kabia kwetu ... tunabakwa ovyo  ovyo  usiku  , wengine  'tumeolewa'  pia  ni  walevi  sasa  haya kweli   ni maisha  tunayostahili  kuishi kama  wanafunzi  tena  wa kike ?" alihoji mmoja wao "Mie  nafikiria  kuacha  masomo  bora  nirudi  nyumbani  kuliko  kuendelea kuishi   kwa  hofu  ya kubakwa usiku  haya  si maisha  haya kidogo," aliongeza.
Wasichana  wa  shule hiyo wanaoishi  katika  'magheto' kijijini  hapo  wamejikuta  wakikabiliwa  na  visa vya  kuvamiwa  na kubakwa  mara kwa mara usiku  ambapo  hivi karibuni  msichana mmoja  alijiua  kwa kunywa sumu ya  panya  baada ya kubakwa  na mtu  asiyejulikana  pia wengine  sita walinusurika  kubakwa   baada ya  kuvamiwa usiku  na watu  wawili wasiofahamika  ambao  waliishia  kuwacharaza marungu mwili  kisha kuwaporoa  kiasi  cha Sh 2,100- taslimu  na kutokomea kusikojulikana.
Habari za kipolisi kutoka Kituo  Cha Polisi  cha Mpui  kilichopo  kilomita 20  kutoka  kijijini  Kaengesa  zinaeleza kuwa  hakuna mtu  yeyote hadi sasa aliyekamatwa  kuhusiana na  tukio hilo  lakini   msako  mkali  unafanyika kuwabaini  watuhumiwa    sheria iweze kuchukua mkondo  wake.

2 comments:

Anonymous said...

Thanks for sharing your thoughts about ပုံစံ.
Regards

Anonymous said...

Everything is very open with a really clear clarification of the challenges.
It was truly informative. Your site is very helpful.
Thank you for sharing!