MKAGUZI ATAKA M-PESA, TIGOPESA, AIRTEL MONEY, EASY PESA ZITOZWE KODI...

Ludovick Utouh.
Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, ameshauri kampuni za simu zinazotoa huduma ya utumaji fedha na kumbi za harusi vitozwe kodi.

Sambamba na hilo aliutaka uongozi wa Bunge, kurejesha Kamati ya Ukaguzi wa Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC).
Alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari baada ya kuwasilisha taarifa yake bungeni mjini hapa jana akisema uamuzi wa kufuta kamati hiyo na kazi zake kuunganishwa na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), hautakidhi matarajio ya wadau wa uwajibikaji.
Kwa upande wa kodi, alishauri kodi kutoka kwa wafanyabiashara wadogo, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ihusishe kikamilifu makatibu kata kutambua walipa kodi wakiwamo wamiliki wa kumbi za harusi na mikutano.
Akifafanua kuhusu kodi kwenye kampuni za simu za mkononi alitaka zitozwe kodi ya zuio la malipo ghafi ya kamisheni, inayolipwa kwa wanaofanya biashara hiyo ya kuhamisha fedha kwa niaba ya kampuni.
Uhamishaji fedha hizo unafanywa kwa kupitia mifumo ya M-pesa, Tigo Pesa, Airtel Money na Easy Pesa.
Alishauri kodi hiyo ya zuio, ipunguzwe kutoka kodi ya mwisho inayotakiwa kulipwa na kampuni za simu.
Utouh alisema PAC itazidiwa na wingi na ukubwa wa majukumu na akatoa mfano, kuwa hata kabla ya kamati hizo kuunganishwa, kamati hizo mbili zilikuwa zinazidiwa.
Alisisitiza kuwa ni jambo jema POAC irejeshwe kwa jina lolote, lakini kazi zake zibaki zile zile.
“Kuna mashirika 176, ukiweka na taasisi za Serikali mzigo unakuwa mkubwa na PAC hii ya Zitto (Kabwe ambaye ni Mwenyekiti), kama atafanikiwa hata nusu ya kazi zake, itakuwa ni muujiza.
“Hivyo nashauri tuone uwezekano wa kurudisha kamati hii hata kama itakuwa na haja ya kubadilisha jina, iitwe ya mashirika ya umma au ya uwekezaji, lakini ifanye kazi za POAC,” alisema Utouh.
CAG pia alisisitiza kuwa licha ya Serikali kufanya mabadiliko ya sheria ya ukaguzi wa umma, mabadiliko hayo hayajaingilia uhuru wa ofisi yake kutimiza wajibu wake.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa PAC, alilalamikia sheria hiyo kuwa inawaziba midomo wabunge kwa vile wanazuiwa kujadili ripoti ya CAG.
Zitto alisema mfumo uliokuwapo wa kuwasilisha ripoti za kamati za Bunge, umefutwa na Serikali baada ya kutunga sheria, na Serikali inachotaka ni Bunge kujadili ripoti hizo kupitia kamati zake kabla ya kujadiliwa na Bunge zima.
Makamu Mwenyekiti wa PAC, Deo Filikunjombe alisema Serikali imetunga sheria hiyo kwa vile haitaki kusimamiwa na Bunge, ila inataka Bunge kiwe chombo cha kujadili tu.
Alisema hilo halikubaliki na akasisitiza kuwa kamwe hawataruhusu ripoti za Kamati ya CAG isijadiliwe bungeni.
“Tunatumia miezi mitatu kuomba fedha za Watanzania, lakini linakuja suala la kuhoji matumizi yake kwa sasa tunanyimwa fursa hii…hatuikubali ni lazima ripoti hizi zijadiliwe na mwenye kuwajibika awajibike kama ilivyotokea mwaka jana,” alisema Filikunjombe.
Mwenyekiti wa PAC wa zamani John Cheyo alisema sheria hiyo mpya ya Ukaguzi wa Umma, inaifedhehesha Serikali na akashauri marekebisho hayo yafutwe na Bunge ili kutoa fursa ya ripoti ya CAG kujadiliwa.
“Tulikuwa tunakwenda mbele sasa na mabunge mengine yalikuwa yanakuja hapa kujifunza namna tunavyoshirikiana  na CAG kusimamia fedha za umma, lakini sheria hii ya sasa inaturudisha nyuma, tusikubali ni lazima ripoti hii ijadiliwe bungeni,” alisema
Cheyo.
Wakati huo huo, CAG alisema ataanza ukaguzi kwenye misamaha ya kodi kwa vile fedha ambazo zingelipwa kutokana na misamaha, ni za Serikali ambazo zinatolewa kama ruzuku kwa wanaopewa misamaha hiyo.
“Tumeamua kuikagua kwa kina misamaha yote ya kodi kuanzia mwaka ujao wa fedha kwa madhumuni ya kuangalia manufaa ya misamaha hiyo kwa uchumi wa Taifa,” alisema Utouh.
Lakini CAG alitaka hati za misamaha ya kodi, ziwekwe bayana kuwa msamaha wa kodi ni wa muda gani, unaanza lini na kumalizika lini.
Alitaka misamaha ya kodi iainishwe ikionesha malengo yanayokusudiwa na kuwa na utaratibu wa Serikali kusimamia utekelezaji wa misamaha hiyo.
Ameshauri pia mikataba yote yenye vipengele vya misamaha ya kodi, ipitiwe na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya ushauri kabla ya kusainiwa na pande husika.
Pia alishauri mikataba ya kuchimba madini, ijadiliwe na Kamati ya Bunge inayoshughulikia masuala ya madini, na ushauri utolewe kwa waziri husika kabla ya kusainiwa.

No comments: